Latest Post

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akisema jambo kwa timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kilichofanyika Wilaya ya Misungwi.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Dkt. Thomas Rutachuzibwa akisema jambo kwa timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kilichofanyika Wilaya ya Misungwi.

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Tiba anayesimamia Hospitali za Rufaa za Mikoa Dkt. Caroline Damian (kulia) pamoja na Katibu wa Mganga Mkuu wa Serikali Bi. Maurine Kunambi (kushoto) wakiwa kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga Mkoa wa Mwanza.

Timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza wakiwa kwenye kikao cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

Timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza wakiwa kwenye kikao cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.


VIFO VYA MAMA WAJAWAZITO HAVIVUMILIKI TENA" – MGANGA MKUU WA SERIKALI

Na Englibert Kayombo WAMJW - MWANZA.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi amesema kuwa Serikali haitovumia tena vifo vya akina mama wajawazito vinavyosababishwa na uzembe wa watumishi kazini.

Prof. Makubi ametoa kauli hiyo alipokuwa akifunga kikao kazi cha timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kilichofanyika Wilayani Misungwi kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

"vifo vya akina mama wajawazito havivumiliki tena kwa sasa hivi kwenye hii dunia ambapo tumeingia uchumi wa kati, ni lazima tutafute mbinu mpya na nzuri tuweze kuziendeleza na kuhakikisha kwamba ambaye amekuja kuleta maisha asifariki” amesema Prof. Makubi.

Amesema siyo vifo vya akina mama wajawazito tuu ndio vizuiwe bali hata vya watoto wachanga wanaozaliwa pia vidhibitiwe kwa wataalam wa afya kuhakikisha watoto hao wanazaliwa salama pia.

Prof. Makubi amesema Serikali imewekeza rasilimali nyingi kwenye sekta ya afya hivyo ni vyema matunda ya uwekezaji huo yakaenda kuonekana kupitia uboreshwaji wa huduma bora za afya ikiwemo kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

Amesema anashangazwa na vifo vingi vya akina mama wajawazito kutokea katika vituo vya kutolea huduma za afya na sio kwenye Jamii na kuwataka watumishi hao kujitafakari ni sehemu gani kuna changamoto ili zifanyiwe kazi na kudhibiti vifo hivyo.

“Nimefurahishwa kuona mmekutana hapa kutafakari, kwa hiyo mmeshaliona tatizo hamkusubiri Wizara ya Afya kuja kuwaambia mfanye nini, hilo ndio linanipa moyo mmejitambua na mmeamua kuchukua hatua wenyewe” amepongeza Prof. Makubi wa timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kwa kuanza kuchukua hatua.

Aidha,Prof. Makubi ametoa wito kwa Mikoa mingine iendeleze kile ambacho mkoa wa Mwanza imeanza kufanya kwa kufanya vikao vya tathimini na kuweka mikakati ya kudhibiti vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga. 

“Kabla ya mwezi wa kwanza haujaisha kila Mkoa uwe umeshakaa, ukishirikisha viongozi wote wa Mkoa, Wilaya na Halmashauri vituo vya afya mpaka zahanati wawe na wawakilishi ili mjadili mbinu ambazo zinaweza kupunguza vifo vya akina mama wajawazito kwa kiasi kikubwa zaidi”

 Amesisitiza Prof. Makubi akitoa agizo hilo kwa timu za uongozi wa afya kwa mikoa yote.“Tuondoke hapa tulipo kwa sababu wananchi wanatamani twende tupige hatua moja mbele ili tukaboreshe huduma zetu, kwa mikakati mliyoweka tukiitekeleza naamini tunaweza tukatoka kwenye tatizo hili” Amesisitiza Prof. Makubi.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Dkt. Thomas Rutachuzibwa amesema kuwa wameyapokea maelekezo yote aliyoyatoa Mganga Mkuu wa Serikali na watayafanyia kazi kuhakikisha vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinadhibitiwa mkoani humo.

“Ninakuahidi ndani ya miezi mitatu tutaanza kupata mabadiliko, tutakaa kwa muda uliobaki kuweka mpango kazi kuhakikisha tunaenda kutekeleza yale yote tuliyopanga ili kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga” amesema Dkt. Rutachuzibwa.

Dkt. Rutachuzibwa amesisitiza suala la wajibikaji kwa watumishi wa afya wakiwa kwenye maeneo yao ya kazi kwa kutambua wana wajibu upi na kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wananchi na kupunguza changamoto zilizopo maeneo yao ya kazi.

“Kila mmoja ajitambue, tutoe huduma kwa wananchi, kuanzia leo naomba wote tuanze upya, kila mtu awajibike kwa kipande chake” amesisitiza Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Thomas Rutachuzibya.

Mwisho


Mkurugenzi wa Huduma za Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe kutoka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Ntuli Kapologwe akisema jambo kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na Uzazi na Watoto wachanga Mkoa wa Mwanza

Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Emmanuel Tutuba akisema jambo wakati wa kikao kazi cha kujadili ivifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kwa mkoa huo

Mganga Mkuu Mkoa wa Mwanza Dkt. Thomas Rutachuzibwa akisema jambo wakati wa kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga katika mkoa huo

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Tiba anayesimamia Hospitali za Rufaa za Mikoa Dkt. Caroline Damian (kushoto) pamoja na mwakilishi kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Serikali Bi. Maurine Kunambi (kulia) wakiwa kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga Mkoa wa Mwanza.

Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Benjamin Mkapa (kulia) Dr. Ellen Mkondya- Senkoro pamoja na viongozi wengine wakiwa kwenye kikao kazi cha kujadilii vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga Mkoa wa Mwanza.

Wajumbe wa timu ya afya ya Mkowa wa Mwanza wakiwa kwenye kikao cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga katika Mkoa wa Mwanza.

Na Englibert Kayombo, WAMJW - MWANZA

Watumishi wa kada ya afya nchini wameaswa kuhakikisha wanadhibiti vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kwa kuwajibika ipasavyo wakiwa kazini na kuepukana na tabia za uzembe.

Kauli hiyo imetolewa na na Mkurugenzi wa Huduma za Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe kutoka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Ntuli Kapologwe alipokuwa akizungumza na timu ya afya ya Mkoa wa Mwanza kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kwa mkoa huo.

“Suala la vifo, pasipokuwepo na uwajibikaji na umoja ni vigumu sana kuweza kulifanikisha, kuchukua hatua imekuwa changamoto kwa timu nyingi hivyo kupelea kuongezeka kwa vifo” amesema Dkt. Ntuli.

Ameendelea kusema kuwa wataalam wa afya hawatakiwi kuoneana aibu endapo mjumbe wa timu hatofanya kazi yake ipasavyo kwa uzembe wake mwenyewe achukuliwe hatua za kinidhamu ili kuweza kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kupunguza vifo vya akina mama na watoto wachanga.

Amesema kuwa wataalam wa afya wanapaswa kuwa wamoja na kushirikiana kikamilifu wakiwa kazini na kuacha kusubiri wataalam kutoka ngazi ya juu kuja kutoa maamuzi ya vitu ambavyo vingewezwa kufanywa na viongozi katika eneo husika.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Emmanuel Tutuba amesema vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga vimekuwa viongezeka mkoani humo na kuwataka watumishi wa kada ya afya kuhakikisha wanapunguza kiwango cha vifo hivyo kwa mkoa huo ambao ni kinara wa huduma bora za afya katika Kanda ya Ziwa.

Akitaja takwimu za vifo hivyo, Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Tutuba amesema katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2015 vifo vilikuwa 145, mwaka 2016 vifo 151, mwaka 2017 vifo 193, mwaka 2018 vifo 151, mwaka 2019 vifo 171 na kwa mwaka huu mpaka kufikia mwezi Septemba vimetokea vifo 142.

“Lazima tukae tutafakari, licha ya uwekezaji mkubwa ambao Serikali imefanya lakini vifo vinaongezeka, tunapokutana hivi tusiishie tuu kupashiana, ni lazima tutimize wajibu wetu” amesisitiza Bw. Tutuba.

Hata hivyo Bw. Tutuba amepongeza watumishi wa kada ya afya mkoani humo kwa juhudi zao wanazofanya kuhakikisha wanaokoa maisha ya watanzania pamoja na raia wa kigeni wanaokuja mkoani humo kwa ajili ya huduma za matibabu.

“Tumejitahidi kufanya mazuri mengi, lakini badi hatujatekeleza kwa asilimia 100, tumefanya vizuri lakini bado tungeweza kufanya vizuri zaidi endapo kila mmoja angetimiza wajibu wake” amesema Bw. Tutuba.

Mwisho



Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akihutubia Wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akitoa taarifa ya hali ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI mbele ya mgeni rasmi (Hayupo kwenye picha) wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiteta jambo na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro. 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akipeana mkono na Mkurugenzi wa TACAIDS Dkt. leonard Maboko baada ya kuhutubia wananchi, wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro. 
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akipata taarifa kutoka kwa Mkuu wa kitengo cha tiba na matunzo Dkt. Anath Rwebemberwa katika banda la Mpango wa Taifa wa kupambana na UKIMWI (NACP) ulio chini ya Wizara ya Afya, maendeleo ya jamii, jinsia, Wazee na watoto.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi wakiwa na Mkurugenzi wa Kinga Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi (watano kutoka kushoto) Meneja NACP Dkt. Beatrecy Mutayoba (wamwisho), wakwanza kushoto ni Mkuu wa kitengo cha tiba na matunzo Dkt. Anath Rwebemberwa na wapili kushoto ni Mkuu wa kitengo cha Kinga (NACP) Dkt. Magreth Kagashe.


Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiwa na viongozi wengine Wakiserikali, wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".


WANAOFANYA MAPENZI NA WASICHANA WENYE UMRI MDOGO WAONYWA. 

Na Rayson Mwaisemba WAMJW- Kilimanjaro 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa ametoa onyo kali kwa wanaofanya mapenzi (ngono) na wasichana wenye umri mdogo, hali inayosababisha kuwaharibia malengo yao ya baadae. 

Mhe. Kassim Majaliwa ameyasema hayo leo wakati akiwahutubia wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".

"Nataka niwakumbushe na kutoa tahadhari kwa wale watu wazima mnaofanya mapenzi na vijana wadogo wa kike, ole wenu, ole wenu, ole wenu " ameyasema Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.
Alisema kuwa, takwimu za maambukizi mapya ya VVU zinaonesha kwamba asilimia 40 ya maambukizi hutokea kwa vijana na katika hao asilimia 80 ni vijana wa kike, huku akiweka wazi kuwa, vijana ni kundi linalokabiliwa na changamoto ya maambukizi mapya ya VVU nchini.

Aliendelea kusema, kundi la vijana na hasa wa kike lipo kwenye hatari kubwa zaidi ya kupata maambukizi mapya, huku akidai uchambuzi wa kimazingira kuhusu takwimu hizi unaonesha kuwa sababu za vijana kuwa katika hatari ya maambukizi mapya ya VVU ni pamoja na kuanza ngono katika umri mdogo, vijana wadogo wa kike kuwa na mahusiano ya kingono na wanaume wenye umri mkubwa Matumizi yasiyo sahihi na endelevu ya mipira ya kike na kiume.

Aidha, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, ametoa wito kwa vijana kujitambua na kuthamini maisha yao kwa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU, huku akiwakumbusha kuwa vijana ndio nguvu kazi ya Taifa, na kuwataka wale wanaoishi na VVU waendelee kutumia dawa za ARV kwa ufuasi sahihi bila kuacha ili kufubaza VVU na kuimarisha afya zao. 

"Natoa wito kwa vijana kujitambua na kuthamini maisha yao kwa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU kwa kuwa ninyi ni nguvu kazi na Taifa linawategemea. Na wale wanaoishi na VVU waendelee kutumia dawa za ARV kwa ufuasi sahihi bila kuacha ili kufubaza VVU na kuimarisha afya zao", alisema Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa. 

Nae Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe amesema kuwa, Tanzania na Dunia kwa ujumla imepiga hatua kubwa katika jitihada za kukabiliana na janga la VVU na UKIMWI.

Aliendelea kusema kuwa, kama nchi inavyoelekea kufikia malengo ya Tisini Tatu, changamoto, na vipaumbele vimeendelea kubadilika kutokana na mafanikio ya mwitikio wa mapambano.
Takwimu zinaonesha kuwa wanaume, watoto, vijana wanaopevuka na vijana wadogo, na watu wanaofanya tabia hatarishi, wako nyuma kutambua hali zao, ufuasi hafifu wa tiba, na ufubazaji wa VVU usioridhisha. 

Hata hivyo, Prof. Mabula Mchembe amesema kuwa, Serikali inaendelea na jukumu la kutafiti, kuandika na kusambaza taarifa za kitaalamu zinazochambua na kutoa masuluhisho ya changamoto zitazotumika kuhuisha sera, miongozo na taratibu za huduma na afua za VVU na UKIMWI. 

"Tunalo jukumu sasa, la kutafiti, kuandika na kusambaza taarifa za kitaalamu zinazochambua na kutoa masuluhisho ya changamoto hizi ili sasa yatumike kuhuisha sera, miongozo na taratibu za huduma na afua za VVU na UKIMWI", amesema Prof. Mchembe 

Mwisho.


Mkurugenzi wa huduma za kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi akisisitiza jambo mbele ya Waganga Wakuu wa Mkoa na Waratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.

Mkurugenzi msaidizi wa Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe TAMISEMI Dkt. Paul Chawote akieleza jambo wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.

Meneja Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma nchini Dkt. Zuweina Kondo Sushy akifuatilia neno kutoka kwa Mkurugenzi wa huduma za kinga Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.

Waganga Wakuu wa Mikoa na Waratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma wakimkaribisha mgeni rasmi (hayupo kwenye picha), wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.



Na Rayson Mwaisemba WAMJW- DOM 

Mkurugenzi wa kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi ametoa wito kwa Waganga Wakuu wa mikoa wote kutumia mbinu mbali mbali ili kuutokomeza ugonjwa wa ukoma na Kifua Kikuu nchini Tanzania. 

Dkt. Subi ametoa wito huo leo wakati akifunga Mkutano wa mwaka wa Mpango wa taifa wa kudhibiti kifua Kikuu na ukoma uliohudhuriwa na Waganga wakuu na Waratibu wa kifua Kikuu na ukoma ngazi ya Mkoa, uliofanyika Jijini Dodoma. 

"Tumieni kila liwezekanalo ugonjwa wa ukoma uishe nchini Tanzania, kwa Waganga Wakuu wa Mkoa ambao Halmashauri zenu bado zina maambukizi ya ukoma jipeni ndani ya miaka mitano ugonjwa wa ukoma utoweke nchini " amesema Dkt. Subi. 

Dkt. Subi amesema kuwa, ni muhimu kwa viongozi kutumia takwimu ili kuwasaidia katika kufanya maamuzi sahihi na kwa wakati katika utekelezaji wa majukumu yao, jambo litalosaidia kutokomeza maambukizi ya ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma nchini. 

Aidha, Dkt. Subi ametoa agizo kwa Waganga Wakuu wa mikoa wote kuhakikisha maelekezo na maazimio yaliyotokana na Mkutano huo yatolewe kwa maandishi kwa Halmashauri zote nchini ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kutokomeza ugonjwa wa Ukoma na Kifua Kikuu.

Mbali na hayo, Dkt. Subi ameagiza kuendelea kutoa elimu ya Afya kwa umma kwa wananchi kupitia vyombo vya habari kama vile radio za jamii, mitandao ya jamii, ili kuwakinga wananchi wetu dhidi ya maambukizi ya magonjwa ikiwemo ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma. 

"Toeni elimu ya Afya kwa wananchi, wananchi waelimishwe kuhusu magonjwa mbali mbali katika Jamii ikiwemo ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma, wekeni utaratibu wa vipindi vya Afya kwenye radio za mikoa yenu" amesema Dkt. Subi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi msaidizi wa Idara ya Afya na Ustawi wa Jamii na Lishe TAMISEMI Dkt. Paul Chawote amemhakikishia Mgeni rasmi kusimamia utekelezaji wa maazimio ya Mkutano huo ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kutokomeza maambukizi ya ugonjwa wa Kifua Kikuu na ukoma nchini. 

"Sisi kama Ofisi ya Rais TAMISEMI tumejipanga kusimamia utekelezaji wa maazimio yote ambayo yametokana na Mkutano huo ili kupambana dhidi ya ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma nchini "amesema Dkt. Çhawote. 

Mwisho



Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akifungua Mkutano wa saba wa Afya uliohudhuriwa na Wadau mbali mbali wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi Idara ya Afya ustawi wa Jamii na Lishe Dkt. Ntuli Kapologwe akimkaribisha mgeni rasmi, Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Mabula Mchembe (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa saba wa afya, uliohudhuriwa na Wadau mbali mbali wa afya nchini, Jijini Dodoma

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akipita katika banda la NIMR kujionea shughuli zinazoendelea, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa saba wa Afya uliohudhuriwa na Wadau mbali mbali wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Wadau mbali mbali wa masuala ya Afya waliohudhuria Mkutano wa saba wa masuala ya Afya unaoendelea Jijini Dodoma kujadili namna bora ya kuboresha huduma za Afya nchini.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akiwa na Wadau mbali mbali wa Afya wakati wa  Mkutano wa saba wa Afya unaoendelea Jijini Dodoma.



PROF. MCHEMBE AWAAGIZA WATAALAMU WA SEKTA YA AFYA KUFIKIRIA HUDUMA BORA NA NAFUU KWA WANANCHI

Na Rayson Mwaisemba, WAMJW - DOM 

KATIBU Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe ametoa wito kwa Wataalamu wa Sekta ya Afya nchini kuhakikisha wanafikiria namna ya utoaji huduma bora na kwa gharama nafuu ili wananchi wenye hali zote waweze kuzimudu.

Wito huo ameutoa leo, wakati akifungua Mkutano wa saba wa Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Watumishi kutoka Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wadau mbali mbali wanaojihusisha na masuala ya Afya nchini.

"Ni wajibu wetu sisi, tukiwa kwenye Mkutano huu wa wa Afya kuwaza vyema tunamsaidiaje mwananchi wa hali ya chini kupata huduma bora, zenye unafuu na zinazofikika kila sehemu bila kumuumiza mwananchi" alisema Prof. Mchembe.

Hata hivyo, Prof. Mchembe amesema kuwa, Wizara ya Afya itaendelea kutoa ushirikiano kwa Wadau wote ili kufanikisha utoaji huduma bora na nafuu kwa wananchi, huku akiweka wazi kuwa kama Serikali itatendea kazi mapendekezo na ushauri utakaotokana na Mkutano huo. 

Aidha, Prof. Mchembe amesisitiza kuwa, ni muhimu mijadala itayoendelea katika Mkutano huo kuhakikisha inapita kwenye malengo ya Wizara yakiwemo kupunguza vifo vya mama na mtoto, kupunguza maambukizi ya VVU, TB, Ukoma, 

Mbali na hayo, Prof. Mabula Mchembe amewataka Wataalamu hao kujadili masuala ya kupunguza magonjwa yasiyo yakuambukiza ambayo yanaongeza mzigo kwa Serikali kutokana na gharama za kuyatibu magonjwa hayo, yanayotokana na mtindo wa maisha ikiwemo matumizi ya pombe kupita kiasi, kutofanya mazoezi. 

Naye, Mkurugenzi Idara ya Afya ustawi wa Jamii na Lishe kutoka TAMISEMI Dkt. Ntuli Kapologwe amesema kuwa, Serikali imefanya maboresho mengi sana katika miaka saba iliyopita, huku akiweka wazi kuwa mambo yatakayojadiliwa katika kikao hicho yataendana na mpango mkakati wa Sekta afya unaosimamiwa na Serikali kupitia Wizara ya Afya. 

Pia, Dkt.Kapologwe amesema kuwa, kama wasimamizi wa Sera watahakikisha maazimio yatakayotoka kwenye kikao hicho yanaingizwa kwenye mipango ya utekelezaji kwenye Hospitali zote ngazi ya Wilaya, Halmashauri na zahanati kwa utekelezaji zaidi. 

"Katika kikao hiki, pamoja na maelekezo ambayo utayatoa, sisi tukiwa kama wasaidizi wako tutahakikisha, maelekezo yako pamoja na maazimio utakayotoa katika kikao hiki, tunaenda kuyaingiza katika mipango yetu katika Hospitali za Mikoa, Halmashauri na Zahanati" amesema Dkt. Ntuli Kapologwe. 

Mwisho



Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akifungua Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa Tathmini ya Utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu TAMISEMI anaeshughulikia masuala ya Afya Dkt. Dorothy Gwajima akieleza jambo wakati wa ufunguzi  wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa Tathmini ya Utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akimkaribisha mgeni  rasmi Katibu Mkuu Wizara  ya Afya Prof. Mabula Mchembe (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Wakurugenzi kutoka Wizara ya Afya wakiteta jambo wakati  wa ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Baadhi ya Wakurugenzi wasaidizi kutoka Wizara ya Afya  walioshiriki katika ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Baadhi ya Wadau waliohudhuria ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Wakurugenzi kutoka Wizara ya Afya na Wadau wa Sekta ya Afya nchini walio hudhuria  ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara  ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe, akiwa na Sekretarieti ya mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya.



Na, Rayson Mwaisemba WAMJW- DOM 

SERIKALI, kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeendelea kujidhatiti katika kuboresha utoaji huduma za Afya kwa wananchi ikiwemo kupunguza vifo vya mama na mtoto, uboreshaji wa huduma za chanjo, upatikanaji wa vifaa na vifaa tiba. 

Hayo yamesemwa leo na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe wakati akifungua Mkutano wa 21 wa kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya ulioandaliwa kwa pamoja na Wizara yake na Ofisi ya Rais TAMISEMI ukishirikisha Wadau mbalimbali wa Sekta ya Afya nchini unaoendelea Jijini Dodoma.

Prof. Mchembe amesema kuwa, kikao hicho kina umuhimu mkubwa sana katika Wizara na Sekta ya Afya kwa ujumla kwa sababu ndio kinachoweza kuweka mikakati ya nini kifanyike miaka mitano ijayo, baada ya kupitia mikakati ya miaka mitano iliyopita na kuona mafanikio na changamoto zake.

"Kama Serikali tumefanikiwa kuboresha katika kupunguza vifo vya mama na mtoto,  huduma za chanjo, vifaa na vifaa tiba pamoja na uboreshaji wa utoaji huduma zinazotolewa na Watumishi wa Afya" amesema Prof. Mchembe. 

Aidha,  Prof. Mchembe amesema mpango mkakati wa tano unaoenda kuanza ni matokeo ya ule wa nne ambapo unaangazia mafanikio, na kuboresha maeneo yaliyokuwa na changamoto na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha Sekta ya Afya. 

Naye Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia masuala ya Afya kutoka ofisi ya Rais TAMISEMI Dkt. Dorothy Gwajima amesema kuwa, kama wasimamiaji wa utekelezaji wa Sera katika ngazi za Mikoa na Mamlaka za mitaa wapo tayari kutekeleza maagizo na miongozo itayotolewa kupitia kikao hicho cha tathmini ya Sera kilichohudhuriwa na Wadau wote wa Sekta ya Afya nchini. 

"Katibu Mkuu Wizara ya Afya ameeleza mambo mengi, sisi tupo kama Wadau ambao tunasimamia utekelezaji kwenye ngazi ya Mikoa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa tunasubiri maelekezo  na miongozo ya Kisera ili kwenye kipindi cha miaka mitano ijayo tuweze kutekeleza kwa kasi ile ile" alisema Dkt. Gwajima. 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Sera na Mipango Wizara ya Afya Bw. Edward Mbanga amesema kuwa, kikao hicho cha Sera hupokea mambo yote katika Sekta ya Afya yaliyofanyiwa tathmini na yaliyokubalika kuwa ndio yatakuwa malengo na muelekeo wa Sekta ya Afya nchini. 

Mwisho.


MKRdezign

{facebook#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {twitter#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {google-plus#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {youtube#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {instagram#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL}

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget