August 2020

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi (watatu kutoka kushoto) akikagua taarifa za mgonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC, pindi alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi (watatu kutoka kushoto) akipokea taarifa za hali ya mgonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC, pindi alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo.
Kiwanda cha uzalishaji mitungi ya oksijeni kilichopo katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kaskazini KCMC. 

Baadhi ya mashine za uzalishaji wa gesi ya oksijeni inazotumika katika matibabu  ya wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kaskazini KCMC.


TUSHIRIKIANE KUPAMBANA DHIDI YA MAGONJWA YASIYO AMBUKIZA - MGANGA MKUU WA SERIKALI.

Na WAMJW- KILIMANJARO

MGANGA Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ametoa wito kwa watoa huduma za Afya kushirikiana kwa pamoja kwa kutoa elimu, katika mapambano dhidi ya magonjwa yasiyo ambukiza yanayosababishwa na mtindo wa maisha ikiwemo ulaji usiofaa, matumizi ya vileo na kutofanya mazoezi.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Makubi ametoa rai hiyo wakati alipotembelea Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC kukagua hali ya utoaji huduma za Afya katika Hospitali hiyo kwa wananchi.

Prof. Makubi amesema kuwa, ni muhimu watoa huduma za afya kuungana kwa pamoja kushirikiana kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu magonjwa yasiyo ambukiza (NCD), kupitia njia yakuwafuata wagonjwa katika maeneo yao, jambo ambalo litasaidia kupunguza mzigo wa wagonjwa katika hospitali za Rufaa nchini.

"Mshirikiane kwa pamoja kutoa Elimu ya ufahamu, na kupima angalau mara 2 kwa mwaka juu ya  magonjwa yasiyo ambukiza (NCD) kupitia njia ya kuwafuata wateja katika maeneo yao na kuwafanyia upimaji (outreach program)" alisema Prof. Makubi.

Hata hivyo, Prof. Makubi ametoa rai kwa watoa huduma za afya kuhakikisha wanatoa huduma kwa wakati kwa wagonjwa ili kuepusha msongamano unaoweza sababisha mlipuko wa magonjwa mengine katika hospitali na kupunguza usumbufu kwa wagonjwa.

Aidha, Prof. Makubi ameridhishwa kwa kiasi kikubwa hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo, huku akiwataka kuongeza jitihada ili kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi na kupunguza malalamiko yanayoweza kuepukika kwa urahisi.

"Mimi kwa KCMC, sipati malalamiko mengi sana, simamìeni katika ubora huo, na mhakikishe mnaongeza Juhudi zaidi, na kwa hilo nawapongèza sana sana" alisema Prof. Abel Makubi.

Hata hivyo, Prof. Makubi amewapongeza watumishi wa Hospitali ya KCMC wakiongozwa na Mkurugenzi wao Prof. Gileard Masenga kwa kuanzisha mradi wa uzalishaji wa gesi ya oksijeni, jambo linalosaidia kuongeza mapato na kuokoa kiasi kikubwa cha pesa ambacho kingetumika kununua mitungi ya gesi, na pesa hizo kuelekezwa katika kuboresha huduma kwa wananchi.

Nae, Mkurugenzi wa huduma za tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Maghembe amewataka kutobweteka, katika kuwahudumia wananchi, licha ya kazi nzuri ambayo inaendelea kufanywa na uongozi kwa kushirikiana na Mkoa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa uhakika ubora huduma Wizara ya Afya Dkt. Eliakim Eliud amewataka watoa huduma kuhakikisha wanafuata miongozo ya kujikinga ya utoaji huduma (IPC guidelines) wakati wa kuhudumia wagonjwa ili kujikinga wao na wagonjwa wanaowahudumia.

Mwisho.



Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto Dkt. Leonard Subi, akisisitiza jambo mbele ya Waandishi wa habari wakati alipofanya ziara katika ghara la chanjo lililopo katika Hospitali ta Rufaa ya Mkoa wa Dodoma-General.


HATUNA UHABA WA CHANJO NCHINI: DKT. LEONARD SUBI

Na. Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesema kuwa, haina upungufu wa chanjo wa aina yeyote hivyo kuwataka wazazi/walezi kuwapeleka watoto wao kuwapatia chanjo katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi wakati alipotembelea ghala ya kuhifadhia chanjo iliyopo hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kukagua hali ya chanjo katika mkoa huo.

Dkt. Subi amesema kuwa, chanjo zote aina tisa ambazo zinakinga dhidi ya magonjwa kumi na tatu zipo kwenye ghala hilo“tulikua na upungufu wa aina mbili za chanjo nchini kati ya tisa ambazo tumekuwa tukizitoa lakini, sasa hivi chanjo zote zipo, kwani zimeshawasili hapa nchini na usambazaji unaendelea”, amesema Dtk. Subi

Hata hivyo Dkt. Subi amesema kuwa, upungufu huo wa chanjo ulitokea baada ya Dunia kukumbwa na janga la mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19 ambapo anga zote zilifungwa kwani chanjo husafirishwa kwa mnyororo baridi, kwahiyo huitaji usafiri wa anga.

“Tunamshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kulifungua anga la Tanzania ambapo,  chanjo sasa zimeanza kuingia nchini na hadi sasa mikoa kumi na tatu(13) chanjo hizi zimeshapokelewa kati ya mikoa 26, na mikoa mingine kumi na tatu  ya Tanzania Bara usambazaji unaendelea kupitia Bohari ya Dawa (MSD)”.

Aidha, Dkt. Subi alisema kuwa, usambazaji wa chanjo hizo mbili ambazo wananchi walikua wanazikosa, umeshaanza na watazipata kwa uhakika, huku akielekeza bohari ya dawa nchini (MSD) kuhakikisha chanjo zote  zimefika katika mikoa iliyosalia ya Tanzania Bara ifikapo mwishoni mwa wiki hii.

“Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri wote nchini hakikisheni chanjo hizo mnazipeleka kwenye vituo vyetu  vya kutolea huduma za afya na muwajulishe wananchi kwamba chanjo zipo na zinapatikana bila malipo yeyote, wazazi na walezi pelekeni watoto wenu kupata chanjo katika mikoa yenu”Alisisitiza Dkt. Subi.

Kwa upande wa taarifa iliyotolewa na moja ya chombo cha habari hapa nchini kwa kukosekana kwa chanjo ya kuzuia kuhara (Rota) Dkt. Subi alifafanua kuwa, nchi ya Tanzania haijawahi kukosa chanjo hiyo,huku akiweka bayana kuwa, chanjo zilizopungua kwa mwezi mmoja na nusu ni chanjo ya Polio na Surua-Rubella hali iliyosababishwa na mlipuko wa Covid-19 Duniani, huku akisisitiza kuwa serikali imekua ikinunua chanjo hizo kutoka nchi za Ulaya na Asia.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali inaendelea kutoa fedha za chanjo, na kuweka wazi kuwa hadi sasa  imetoa zaidi ya  shilingi bilioni 18 kwa ajili ya ununuzi wa chanjo  na kuifanya  Tanzania kuendelea kuwa katika kiwango cha juu cha utoaji wa chanjo kwa zaidi ya asilimia 98 kwa miaka sita mfululizo.

Hata hivyo, Dkt. Subi amesema kuwa, Tanzania haijawahi kupata mgonjwa wa kupooza tangu mwaka 1996, jambo linalotokana na  uwepo wa hali nzuri ya upatikanaji wa chanjo, huku akidai kuwa nchi ya Tanzania tayari imepata cheti cha utambuzi kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) mwaka 2015.

 

MWISHO.



Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akiwasalimia wagonjwa waliokuwa wakisubiri huduma katika eneo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.

Mkurugenzi wa tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akimjulia hali moja kati ya wagonjwa waliofika kupata huduma za Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara, pindi alipofanya ziara katika Hospitali hiyo.
Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe (wa katikati) akiwa pamoja na  Mkurugenzi wa uhakiki ubora wa huduma kutoka Wizara ya Afya Dkt.  Eliakim Eliud wakikagua muongozo  wa utoaji huduma kwa kwa Wauguzi, pindi walipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.


Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akiwa na Wataalamu wa Maabara katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.
 
Mkurugenzi wa tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akiwa na Wataalamu wa Maabara katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara,  wakati alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za Afya katika Hospitali hiyo.

Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akikagua kadi inayoonesha hali ya idadi ya dawa zilizopo (Bin Card) katika chumba cha kuhifadhia dawa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.

 

WATOA HUDUMA WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA WELEDI KWA KUZINGATIA MAADILI.

Na Rayson Mwaisemba, WAMJW- MANYARA

MKURUGENZI wa tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe ametoa wito kwa Watoa huduma za Afya nchini kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia maadili wakati wa kumhudumia mgonjwa.

Dkt. Grace Magembe ametoa rai hiyo leo, wakati alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za afya, na ujenzi wa miundombinu katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.

Dkt. Grace amesema kuwa, kwa kiasi kikubwa Serikali imewekeza kwenye ujenzi wa miundombinu, vifaa tiba na hali ya upatikanaji wa dawa, ikiwa ni sehemu ya maboresho ya utoaji huduma za afya bora kwa mwananchi katika jamii.

"Serikali imewekeza kwenye miundombinu, kwenye vifaa tiba, hali ya upatikanaji wa dawa, lakini Watumishi wanatakiwa wafanye kazi kwa weledi kwa kuzingatia maadili ya kazi zao wakati wa kumuhudumia mgonjwa " alisema Dkt. Grace.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali imekuwa ikisisitiza sana, kuhusu maadili mazuri wakati wa utoaji huduma kwa wateja, pindi wanapokuja kupata huduma, hii inajumuhisha mapokezi yake, muda anaotumia kusubiri huduma, muda wa kurejesha majibu yake na kauli zinazotumika wakati wa utoaji huduma.

Hata hivyo, Dkt. Grace ametoa wito kwa viongozi wa hospitali kuwa na mpango madhubuti wa matengenezo ya vifaa tiba ili kuepuka ewezekano wa kusimama kwa baadhi ya huduma, hali itayopelekea wananchi kukosa huduma na upotevu wa mapato.

"Kitu kingine ambacho tunasisitiza katika hospitali ni kuwa na mpango madhubuti wa matengenezo ya vifaa tiba, vifaa ambavyo vimenunuliwa na Serikali ni vya gharama kubwa mnoo, fedha nyingi sana zimetumika, kwahiyo tunasisitiza kuwa na mpango wa matengenezo" alisema

Aidha, Dkt. Grace kwa kiasi kikubwa ameridhishwa na hali ya upatikanaji wa dawa katika maeneo alipofanya ziara, huku akitoa rai kwa Watoa huduma kuhakikisha mgonjwa anapoandikiwa dawa azipate dawa alizoandikiwa lakini pia azipate kwa kwa muda sahihi.

" tumeangalia tena suala la upatikanaji wa dawa, namna dawa inavyohifadhiwa, namna dawa inavyotumika, namna dawa inavyotoka chumba cha kuhifadhia mpaka inapomkuta mhitaji wodini, hii yote tumeifanyia kazi kwasababu tunataka hizo dawa zitumike kulingana na mahitaji yaliyotakiwa" alisema Dkt Grace.

Mbali na hayo, Dkt. Grace amesisitiza agizo la Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi juu ya kufanya kazi kwa juhudi na ushirikiano ili kupunguza vifo vya mama na mtoto, huku akisisitiza kuwa, kuweka mikakati thabiti katika mapambano dhidi ya vita hii, na kuweka wazi kuwa vifo vya mama na mtoto vitakuwa ni kigezo cha kuangalia uwajibikaji na utendaji kazi wa Waganga Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Waganga wafawidhi.

"Hatutaki kuona mama wa Kitanzania anakufa wakati analeta kiumbe Duniani, vifo vingi vinasababishwa na sababu ambazo zinaweza kuzuilika, lazima kila Mtumishi afanye kazi, kuanzia Mganga Mkuu wa Mkoa, Mganga Mkuu wa Wilaya, hospitali zote zilizopo ndani ya Mkoa wake, wote wafanye kazi kwa kushirikiana, wake na mkakati, sisi kama Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI tutaendelea kufuatilia tuone kama vifo vinapungua au la na hatua zitachukuliwa " alisema.

Nae, Mkurugenzi wa uhakiki ubora huduma Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Eliakim Eliud amesisitiza kuwa, kuongeza kazi za utoaji huduma kwa kuzingatia ubora wa huduma na kufuata miongozo ya kujikinga wakati wa kuwahudumia wagonjwa.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara Dkt. Damas Kayera ameweka wazi kuwa, Mkoa wa Manyara umeendelea kuwa ma rekodi nzuri juu ya hali ya upatikanaji wa dawa muhimu wa kufikia wastani wa 91%, jambo lililosaidia kupunguza malalamiko kwa wananchi wanaokuja kupata huduma.

"Mkoa unaendelea kuwa na rekodi nzuri ya ongezeko la dawa muhimu, zinazofuatiliwa na Wizara ya afya kwa kila kituo, ambapo kwa kipindi cha nusu mwaka 2020 kumekuwa na wastani wa 91%" amesema.

Mwisho.







Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto-Idara Kuu Afya Edward Mbanga akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi kwenye ukumbi wa Cathedral jijini Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsai, wazee na Watoto akiongea na viongozi  hao wakati wa kikao cha mafunzo ambapo aliwataka kuweka dhamira na malengo  ya dhati  katika kuboresha maadili katika taaluma ya uuguzi na ukunga.

Muuguzi Mkuu kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI Charles Kadugushi akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Uuguzi na Ukunga kutoka Wizara ya Afya Bi. Ziana Sellah akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Msajili wa Baraz a la Uuguzi na Ukunga Agnes Mtawa akiwasilisha mada wakati wa kikao kazi hicho kinachofanyika jijini Dodoma.

Picha ya pamoja ya mgeni rasmi na wasajili wa mabaraza ya kitaaluma yaliyopo chini ya wizara ya afya.

Mgeni rasmi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wauguzi wakuu wa Wilaya mara baada ya ufunguzi.


WAUGUZI NA WAKUNGA WATAKIWA KUTUMIA UTAALAMU WAO KWA AJILI YA USTAWI WA TAIFA

Na.Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Wauguzi na Wakunga nchini wametakiwa kutoa huduma kwa kuzingatia miongozo iliyopo wakati wakitoa huduma kwa weledi ili kufikia malengo na matumaini ya wateja kwa ajili ya ustawi wa Taifa.

Rai hiyo imetolewa leo na Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto – Idara Kuu ya Afya Bw. Edward Mbanga wakati wa ufunguzi wa  kikao kazi  cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi wauguzi wakuu wa wilaya kinachofanyika jijini Dodoma.

Bw. Mbanga amesema  kuwa wauguzi na wakunga ndio watendaji wakuu katika vituo vya afya kwenye ngazi ya jamii hadi Taifa hivyo uwajibikaji mzuri na utawala bora utaboresha utendaji hali itayosaidia kufikia malengo mbalimbali waliyojiwekea katika ngazi zote.

"Viongozi mnatakiwa kuwa wabunifu, wachapa kazi, wenye nidhamu na mfano bora wa kuigwa katika utekelezaji wa majukumu yenu,kwahiyo  ni lazima msimamie utoaji wa huduma uliyo mzuri na wenye heshima na utu.”Alisema

Aidha, Kaimu Katibu Mkuu huyo aliwakumbusha  washiriki hao kuwa, suala la huduma za uuguzi na ukunga ni suala la  ubinadamu zaidi na kuvaa viatu vya wagonjwa wao.

“Hakuna aliyegongwa muhuri wa kuugua  au kuwa mgonjwa akalazwa ,sisi sote ni wagonjwa watarajiwa kwahiyo kama ambavyo sisi tungependa kuuguzwa vizuri, kijibiwa kwa kauli nzuri basi tuhakikishe tunasimamia maadaili ya kazi”.Alisisitiza Mbanga.

Hatahivyo alisema kuwa, Serikali inawahakikishia itaendelea kufanya kazi pamoja na waauguzi  kwa kutoa miongozo thabiti na kuhakikisha upatikanaji wa nyenzo muhimu katika hospitali na vituo vya kutolea huduma ya afya na kuboresha mazingira ya kazi yaliyo bora na salama.

Aliendelea kusema kuwa, hivi karibuni kumekuwa na malalamko  mbalimbali ya kiutendaji  na kitaaluma kutoka kwa wateja  wanaofika kupata huduma za afya na hivyo kuleta taswira mbaya  kwa taaluma yao na kuonyesha hakuna usimamizi mzuri wa utoaji huduma za uuguzi na ukunga.

“Tungependa  wateja wetu watoe sifa  badala ya malalamiko hivyo kikao hiki mje na mipango ya kuondokana na malalamiko kwani taaluma yenu ni zaidi taaluma." alisema.

Hata hivyo, amewakumbusha  viongozi hao kuwa mstari wa mbele kupambana dhidi  ya rushwa na kuhakikisha inatokomezwa katika maeneo yao ya kazi kwani rushwa imekuwa ikilalamikiwa na kuripotiwa katika kada ya afya nchini.

-MWISHO-



MKRdezign

{facebook#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {twitter#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {google-plus#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {youtube#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL} {instagram#YOUR_SOCIAL_PROFILE_URL}

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget